FIGHT FOR FREEDOM

FIGHT FOR FREEDOM

W AZIRI AOMBA DINI ZIELIMISHE KUHUSU MITANDAO YA KIJAMII






VIONGOZI wa dini nchini wametakiwa kutumia nafasi zao kuelimisha umma kuhusu matumizi sahihi ya huduma ya mitandao ya kijamii ili kujiletea maendeleo.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa wakati wa futari iliyoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kushirikiana na Kamati ya Amani ya Mkoa wa Dar es Salaam.
Alisema ni vema viongozi wakatumia nafasi zao kueleza matumizi sahihi na huduma za mitandao ya kijamii katika kueneza imani na kujiletea maendeleo binafsi na taifa kwa jumla.
Waziri Mbarawa alitoa mfano wa machafuko ya nchi ya Misri ya mwaka 2011 yaliyodumu hadi sasa kuwa yametokana na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii kutokana na ujumbe wa mtu mmoja aliouandika kwenye ukurasa wake wa Facebook.
Mwenyekiti wa Kamati ya Amani ya Mkoa wa Dar es Salaam, Shehe Alhad Mussa Salum alisema Kamati yao imefanya mambo mengi kuhakikisha kunakuwapo amani na utulivu nchini.
Shehe Salum alitumia fursa hiyo kuwataka Waislamu kutumia kipindi cha Mfungo wa Mwezi Mtukufu Ramadhan kuleta amani miongoni mwa watu wa imani na dini mbalimbali. Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, James Kilaba alisema ukuaji wa teknolojia umekuja na changamoto nyingi zinazohitaji ushirikiano na wadau mbalimbali kuzishughulikia.