FIGHT FOR FREEDOM

FIGHT FOR FREEDOM
Showing posts with label kitaifa. Show all posts
Showing posts with label kitaifa. Show all posts
MZAZI ATUPWA JELA MIKA 30 KWA KUZAA NA BINTI YAKE

MZAZI ATUPWA JELA MIKA 30 KWA KUZAA NA BINTI YAKE



Mahakama ya wilaya ya Misungwi jijini Mwanza imemuhukumu baba mmoja kwenda jela kutokana na kukutwa na hatia ya kumzalisha mtoto wake wa kumzaa.

Mzazi huyo, Jacob Shabani (30) mkazi wa Kijiji cha Wanzamiso, Misungwi alihukumiwa kwenda jela miaka 30 kwa kosa la kufanya mapenzi na mwanaye wa kuzaa akiwa na umri wa miaka 14.

Akitoa ushahidi wake mahakamani hapo mtoto huyo alisema “Baba alinipa ujauzito mara tatu, nilizaa mara mbili mtoto mkubwa alifariki mwaka jana kesi ilipokuwa imeanza, mimba moja iliharibika baada ya kunipiga sana, na sasa nina mtoto mdogo ana mwaka mmoja.”.

Mtoto huyo amesema hali hiyo ilitokea baada ya baba yake kutengana na mama yake kuondoka nyumbani wakati yeye akiwa na miaka 12 mwaka 2015 na ndipo baba yake aliza kufanya naye mapenzi.

Kwa upande mwingine, mzazi huyo ameiomba mahakama hiyo impunguzie adhabu hiyo akidai kuwa yeye ni mzazi na anafamilia inamtegemea

Mjadala wa bajeti kutikisa bunge siku 7




BAADA ya maoni ya wasomi, wanasiasa, taasisi kadhaa na wananchi wa kawaida, mjadala wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/18 unahamia bungeni.
Kuanzia leo kwa siku saba hadi Juni 20, mwaka huu, wabunge watajadili kabla ya kuamua kwa kura ya wazi kupitisha Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/18 iliyowasilishwa bungeni Alhamisi iliyopita. Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango aliwasilisha bungeni Bajeti ya Serikali yenye thamani ya Sh trilioni 31.7 zinazotarajiwa kukusanywa na kutumika kuanzia Julai mosi, 2017 hadi Juni 30, 2018.
Dk Mpango alisema jumla ya mapato ya ndani, yakijumuisha mapato ya halmashauri, yanatarajiwa kuwa Sh trilioni 19.977.0, sawa na asilimia 63.0 ya bajeti yote. “Kati ya mapato hayo, serikali inalenga kukusanya mapato ya kodi ya jumla ya shilingi bilioni 17,106.3 sawa na asilimia 85.6 ya mapato ya ndani. “Aidha, mapato yasiyo ya kodi ni shilingi bilioni 2,183.4 na mapato kutoka vyanzo vya halmashauri ni shilingi bilioni 687.3,” alieleza Dk Mpango.
Alisema Washirika wa Maendeleo wanatarajiwa kuchangia Sh trilioni 3.971.1 ambayo ni asilimia 12.5 ya bajeti yote, ambayo imepokewa kwa pongezi nyingi na wasomi, wachumi, wananchi wa kawaida na wanasiasa mbalimbali waliotoa maoni yao baada ya kuwasilishwa. Miongoni mwa mambo yaliyowafurahisha wengi katika bajeti hiyo ni kufutwa ada ya kila mwaka ya leseni ya magari; kufuta ada ya ukaguzi wa viwango vya mazao ya biashara; kutoza kodi ya VAT kwa kiwango cha sifuri kwa huduma zinazotolewa kwenye usafirishaji wa bidhaa/mizigo nje ya nchi.
Pia kuwatambua rasmi wafanyabiashara wadogo wasio rasmi kama machinga, mama lishe, wauza mitumba; kutoza ushuru wa forodha kwa kiwango cha asilimia 0 badala ya asilimia 25 kwenye malighafi na vifaa vinavyoagizwa nje kwa ajili ya kuunganisha na kutengeneza vifaa ambavyo ni mahsusi kwa ajili ya matumuzi ya walemavu. Pia kutoa msamaha wa kodi, riba na adhabu zinazoambatana na madeni yote (Tax Amnesty) ya ada ya leseni ya magari, ni eneo jingine lililowafurahisha wananchi wengi pamoja na wabunge.
Kupigwa marufuku kwa kusafirishwa kwa madini kutoka mgodini hadi moja kwa moja nje ya nchi, pia ni eneo jingine lililowagusa watu wengi hasa wakati huu ambao imebainika kuwa rasilimali ya madini inaibwa kwa kiasi kikubwa na wawekezaji wa migodi nchini. Mambo mengine mazuri ya bajeti ni kuondolewa kwa kodi katika masuala ya mafuta ya kula, vyakula vya mifugo na mbolea, na hivyo kuleta unafuu mkubwa kwa wakulima na wafugaji pamoja na Watanzania wanaoendesha viwanda vya kusindika mafuta ya kula.
Wabunge wengi hasa wale wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) walionesha kufurahishwa na bajeti hiyo wakati ikisomwa na Dk Mpango. Mara kadhaa walimfanya asite kuendelea kuisoma kutokana na kumkatisha kwa nderemo na vifijo na wengine wakirukaruka walipokaa na kupiga meza kuonesha bajeti imekata kiu yao. Hata Spika wa Bunge, Job Ndugai alifikia mahali akasema ni vyema angewahoji wabunge kama waziri asiendelee kuisoma maana bajeti hiyo imejibu kila kitu. Baada ya Dk Mpango kumaliza saa 2.09 za kuisoma bajeti hiyo ya pili ya uongozi wa Rais John Magufuli, Spika Ndugai alikazia kwa kusema, “Haijapata kutokea.”
Kwa hiyo, kwa siku saba kuanzia leo, wabunge watapata fursa ya kukazia kile walichokuwa wakikifurahia bungeni wakati bajeti ilipokuwa inawasilishwa kwao. Matarajio ya wengi ni kwamba mjadala hautakuwa mkali sana, ingawa yapo maeneo wabunge wanaweza kuishauri serikali kuendelea kuyaboresha kwa nia ya kuwapa unafuu wananchi wanyonge ambao Rais Magufuli amejitanabaisha kuwa anakusudia kuwakomboa. Kwa mujibu wa Spika Ndugai, mjadala wa leo utaanza kwa kupokea maoni ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Hawa Ghasia ambaye ni Mbunge wa Mtwara Vijijini (CCM).
Kamati hiyo kwa takriban siku tano ilifanya mashauriano na serikali kuhusu mwelekeo wa bajeti hiyo baada ya wabunge kumaliza kujadili na kupitisha bajeti za kisekta. Akimaliza mwenyekiti huyo wa Bajeti, itakuwa zamu ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuwasilisha maoni yake kabla ya wabunge wengine kutoa maoni yao. Wakati huo huo, Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TSPF), imeipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuwasilisha bajeti nzuri bungeni wiki iliyopita. Akizungumza katika Kongamano la Pili la Uwezeshaji mjini hapa juzi, Mkurugenzi wa Sera, Utafiti na Uwezeshaji wa TSPF, Gili Teri alisema bajeti ina mambo mengi mazuri.
Aliyataja baadhi ya mambo hayo ni kupunguzwa kwa kiwango cha Kodi ya Mapato ya Makampuni kutoka asilimia 30 hadi 10 kwa miaka mitano kuanzia mwaka mwekezaji atakapoanza uzalishaji. Teri alisema hali hiyo itasaidia sana katika ushindani kwenye uwekezaji hasa kwa wawekezaji wa viwandani. Alieleza uzuri mwingine wa bajeti hiyo ni kwenye kodi zilizoondolewa katika mafuta ya kula, mbolea na vyakula vya mifugo, kwamba itawasaidia Watanzania katika kushiriki kwenye uchumi wa viwanda. Upinzani wadai bajeti ina mapungufu Kambi ya upinzani imesema jana kuwa bajeti ya mwaka huu ina mapungufu mengi na makubwa na imelenga kumnyonya mwananchi maskini.
Hotuba ya Upinzani inatarajiwa kuwasilishwa na Mbunge wa Mbozi, Joseph Silinde badala ya Waziri kivuli wa Fedha na Mipango, Halima Mdee ambaye amefungiwa kutohudhuria shughuli za kibunge kwa mikutano mitatu ya bunge. Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, Mdee alisema bajeti hiyo ina mapungufu mengi na makubwa na maoni ya kambi hiyo yatawasilishwa kwenye kitabu chenye kurasa 200.
Alisema baada ya kufanyika uchambuzi wa kina wa bajeti, iliyowasilishwa na kugundua mapungufu kadhaa ikiwemo kwani bajeti hiyo ambayo takwimu za vitabu vyake vya mapato na matumizi (Volume 1,11,111 na 1V) zinatofautiana sana, pia sura ya bajeti iliyosomwa na Waziri wa Fedha na Mipango inatofautiana pia na vitabu hivyo. Mdee alisema kitabu cha mapato ya serikali, kinaonesha kuwa serikali kwa mwaka wa fedha 2017/2018 ilikusanya jumla ya Sh trilioni 23.9, kitabu cha matumizi ya serikali kinaonesha kuwa serikali inakusudia kutumia jumla ya Sh trilioni 26.9 ikiwa ni ongezeko la matumizi ya Sh trilioni tatu ambayo vyanzo vyake havikuoneshwa kwenye kitabu cha mapato.
“Wakati huo huo sura ya bajeti iliyosomwa na waziri wa fedha inaonesha bajeti ya serikali kwa maana ya mapato na matumizi ya mwaka wa fedha 2017/2018 ni kiasi cha Sh trilioni 31.7 kiasi ambacho hakionekani popote kwenye mapato na matumizi ya serikali. Pia alisema kwa mujibu wa mpango wa taifa wa maendeleo wa miaka mitano tarakimu ya Sh trilioni 31.7 inaonekana kwamba ni makisio ya bajeti ya serikali ya mwaka wa fedha 2018/2019. Alisema mambo kama hayo yanaonesha mkanganyiko katika bajeti hiyo.
“Hii ni bajeti ambayo imedhamiria kuua kabisa dhana ya ugatuaji madaraka kwa serikali za mitaa kwa kuziondolea serikali za mitaa madaraka yake ya kisheria ya kukusanya kodi ya majengo, kodi ya mabango na ushuru wa huduma mijini kwa malengo ya kujiendesha na kurudisha madaraka hayo ya ukusanyaji kodi hizo serikali kuu kupitia TRA,” alisema. Mdee alisema hiyo ni bajeti ambayo kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, inawalipisha Watanzania maskini wasio na uwezo wa kumiliki magari kodi ya ada ya mwaka ya leseni za magari kwa kuihamishia kodi hiyo kwenye ushuru wa bidhaa za mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa ambapo athari zake ni kupanda kwa nauli katika sekta ya usafirishaji.
Alisema jambo hilo litasababisha kupanda kwa bei za vyakula, kupanda kwa bei za kusaga na kukoboa nafaka kwa kutumia mashine zinazotumia petrol na dizeli kwa wananchi waishio vijijini. Pia alisema kuwa wananchi maskini watapata changamoto kwani wengi wanatumia mafuta ya taa kwa ajili ya kupikia na matumizi mengine ya nyumbani. Pia alisema bajeti hiyo kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania serikali itatoza kodi ya Sh 10,000 kwa nyumba zote katika halmashauri zote nchini zikiwemo nyumba za tembe na tope.
“Hii ni bajeti ambayo imeendelea kupandisha kodi kwenye bidhaa ambazo uzalishaji hutumia malighafi inayozalishwa ndani ya nchi. Alisema kambi rasmi ya upinzani bungeni itatoa vipaumbele katika sekta ya elimu ambayo itatengewa asilimia 20 ya bajeti ya maendeleo, sekta ya viwanda itatengewa asilimia 15, sekta ya nishati asilimia 15, sekta ya kilimo asilimia 10 na sekta nyingizo zitapata asilimia 40 iliyobaki bajeti ya maendeleo. Alisema vipaumbele hivyo vikitekelezwa kwa ukamilifu Tanzania itapunguza umaskini kwa asilimia 50 kwa kuwa ni vipaumbele vitakavyochochea ajira kwa watu wengi.

Magufuli: Hakuna mchanga wa madini utakaotoka kwenda nje ya nchi







RAIS John Magufuli amesema kwa sasa hakuna mchanga wa madini utakaotoka kwenda nje ya nchi huku akiitaka kampuni ya uchimbaji madini nchini Acacia kutubu na kukubali makosa yake kama inataka kuendelea kufanya biashara nchini.
Ameagiza mamlaka zinazohusika kuiita kampuni hiyo na kabla ya jambo lolote inapaswa kuilipa serikali fedha kwa kuwa imefanya udanganyifu kwa muda mrefu, wakishakubali hayo tunaweza kukaa kwa makubaliano. Ametoa kauli hiyo baada ya kupokea ripoti ya kamati ya pili iliyoundwa kuchunguza mchanga wa madini uliokuwa ukisafirishwa kwenda nje ya nchi, huku akiwataka wanasheria kuungana pamoja kwaajili ya maslahi mapana ya Tanzania.
“Kwa kampuni hii inayojiita Acacia, muwaite kwanza muwadai hela zetu, kabla hata ya kusajili, wakubali kwamba tuliwaibia na tubatubu na tunalipa, tuko tayari kukaa kwa makubaliano, ninasema kwa sasa hakuna mchanga utakaotoka kwenda nje,” amesema rais Magifuli.
Aidha, Rais Magufuli amemuagiza Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi kuunda timu ya wanasheria waaminifu ambao watapitia na kuzifanyia marekebisho sheria zote zinazohusu mikataba ya madini ili zipelekwe bungeni kwaajili ya kujadiliwa na kufanyiwa marekebisho.
Amesema kuwa sheria hizo zinapaswa zipelekwe bungeni hata kama ni kwa bunge kuongezewa muda ili ziweze kujadili nakufanyiwa marekebisho kwa maslahi mapana ya Taifa. Aidha ameelezwa kushangazwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kushindwa kuwa na rekodi ya usafirishwaji wa dhahabu pamoja na Wizara ya Nishati na Madini kufanya kazi na kampuni ya Acacia bila kujua kama haijasajiliwa.
“Ukiwa na mali yako kwa mfano umepeleka pamba Ulaya, unapata rekodi kwamba safari hii tumepeleka tani kadhaa, je dhahabu, tunaona ni ya hovyo tu…Wizara yaNishati haikujua kama inafanya kazi na mtu ambayo hajasajiliwa, unafanya nae kazi toka mwaka 1997, unawatuma TMAA wakamkague, hata siku moja hujawahi kumwambia wewe cheti chako kiko wapi,” amesema.

Waziri Mpango ataja vipaumbele vya Serikali katika bajeti ya 2017/18



Serikali imeainisha maeneo ya kipaumbele kwa mwaka 2017/2018 kulingana na mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka ujao wa fedha.

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango amesema hayo leo Bungeni mjini Dodoma alipokuwa akiwasilisha Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2017/2018.

Dkt. Mpango amevitaja vipaumbele hivyo kuwa ni pamoja na miradi ya kielelezo ya maendeleo ambayo inayolenga kufanikisha utekelezaji wa Malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 ni pamoja na miradi ya Makaa ya Mawe Mchuchuma, Mchuchuma Liganga, ujenzi wa reli ya kati kutoka Dar es salaam, Tabora hadi Kigoma yenye urefu wa km 1,251 kwa “Standard Gauge” pamoja na matawi yake ya Tabora kupitia Isaka hadi Mwanza yenye urefu wa km 379, Isaka hadi Rusumo km 371, Kaliua kupitia Mapanda hadi Karema km 321, Keza hadi Ruvubu km 36 na Uvinza hadi Kelelema kuelekea Musongati yenye urefu wa km 203.

Miradi mingine ya kielelezo ni uboreshaji wa Shirika la Ndege TAanzania (ATC), ujenzi wa mitambo ya kusindika gesi mkoani Lindi, uanzishwaji wa Kanda Maalum za Kiuchumimkoani Tanga, Bagamoyo, Kigoma, Ruvuma, uanzishwaji wa kituo cha biashara cha Kurasini, kusomesha vijana katika stadi za mafuta na gesi, uhandisi na huduma za afya.

Waziri Dkt. Mpango ameyataja maeneo mengine ya kipaumbele kuwa ni viwanda vya kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa kukuza uchumi wa viwanda, kufungamanisha maendeleo y uchumi na maendeleo ya watu, mazingira ya wezeshi kwa uendeshaji biashara na uwekezaji, ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi pamoja na maeneo mengine muhimu kwa ukuaji wa uchumi na ustawi wa taifa.
Dkt. Mpango amesema kuwa shabaha ya uandaaji wa mpango wa bajeti ya mwaka 2017/18 unaongozwa Serikali kusimamia mambo ya uchumi kwa ujumla ikiwemo kuongeza kasi ya ukuaji wa pato halisi la taifa kufikia asilimia 7.5 kwa mwaka 2017, asilimia 7.9 mwaka 2018 na asilimia 8.2 mwaka 2019, kudhibiti kasi ya mfumuko wa bei na kuhakikisha kuwa unabaki kwenye wigo wa tarakimu moja kufikia asilimia 5.0 katika kipindi cha muda wakati, kuwa na pato ghafi la taifa la sh. trilioni 123.9 kwa mwaka 2017/18, sh. trilioni 139.7 kwa mwaka 2018/19 na sh. trilioni 165.4 mwaka 2019/20 pamoja na mapato ya kodi kufikia asilimia 14.6 ya pato la taifa mwaka 2017/18, asilimia 15.5 mwaka 2018/19 na asilimia 15.8 mwaka 2019/20.

Aidha, ametaja misingi ya mpango na bajeti kuwa ni amani, usalama, utulivu na utangamano wa ndani ya nchi na nchi jirani ambavyo vitaendelea kudumishwa nchini.
Kuhusu mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2017/2018, Dkt. Mpango amesema amewaagiza Maafisa Masuuli kuzingatia masuala muhimu wakati wa uandaaji wa mipango na bajeti za mafungu yao ili kutekeleza Sheria ya Bajeti Na. 11 ya mwaka 2015.
Zaidi ya hayo, Dkt. Mpango amesisitiza uwepo usimamizi na udhibiti wa matumizi, ulipaji na ongezeko la madeni ya Serikali, ukusanyaji wa mapato pamoja na mfumo wa utoaji taarifa za utekelezaji.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti Hawa Ghasia alipokuwa akitoa taarifa ya kamati yake amesema kuwa Kamati yake inardhishwa na hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kusimamia Sheria ya Bajeti na kanuni zake ambayo inahakikisha usimamizi na uwajibikaji katika hatua zote za mchakato wa bajeti unazingatiwa.

Naye Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni Halima Mdee alipokuwa akiwasilisha hotuba yake amesema kuwa Kambi Rasmi inaunga mkono hatua za kisheria zinazochukuliwa na Serikali kwa wale wote waliohusika kwa namna moja au nyingine kuhujumu uchumi wa nchi.
Mkutano wa Tano wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uanatarajiwa kuhitimishwa Novemba 11 mwaka huu huku shughuli mbalimbali za kuishauri Serikali zikiwasilishwa kupitia mijadala ya Wabunge.






Serikali yaokoa bilioni 54/-katika rushwa




WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Serikali imefanikiwa kuokoa Sh bilioni 53.9 kutokana na uchunguzi na operesheni mbalimbali zilizofanywa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) katika mwaka 2016/2017.
Amesema kiasi hicho cha fedha ni kikubwa mno, ikilinganishwa ni Sh bilioni 7 tu zilizookolewa katika mwaka 2015/2016. Alisema hayo jana wakati akifungua semina ya Mtandao wa Wabunge wa Afrika walio katika Mapambano ya Rushwa (APNAC) Tawi la Tanzania kwenye ukumbi wa African Dream mjini Dodoma.
Akizungumzia hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika mapambano dhidi ya rushwa, alisema Serikali imeanza kupata mrejesho mzuri kwamba watumishi wa umma wanawajibika ipasavyo na vitendo vya rushwa vinaendelea kupungua.
“Baadhi ya hatua tulizochukua ni pamoja na kuimarisha taasisi yetu ya TAKUKURU; kuimarisha matumizi ya mashine za kielektroniki ili kupunguza mianya ya kupoteza mapato; kuanzisha mahakama ya mafisadi; kusimamia nidhamu katika utumishi wa umma na kuchukua hatua za haraka za kinidhamu na za kisheria dhidi ya watuhumiwa wote wa rushwa na ufisadi,” alisema.
Aliwaomba wabunge waendelee kuiunga mkono Serikali, kwani haina mzaha kwenye mapambano hayo. “Serikali haina mzaha kwenye mapambano dhidi ya rushwa na tutaendelea na mapambano hayo.
Hivyo, ninaomba waheshimiwa wabunge muendelee kutuunga mkono katika mapambano haya, twende kwa wananchi tukatoe wito kwao watuunge mkono kwenye vita hii,” alisisitiza.
“Tayari tumefanya tathmini na kubaini mianya ya rushwa katika sekta za ardhi, uchukuzi, biashara na maji na hivyo kuziba mianya hiyo. Tutaendelea kuiwezesha TAKUKURU ili iendelee na kazi nzuri waliyoianza ya kubaini mianya na kutoa ushauri wa kuziba mianya hiyo ya rushwa.
Lengo letu ni kuwekeza zaidi kwenye kuzuia, kwa kuwa kinga ni bora kuliko tiba”. Mapema, akizungumza katika semina hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais anayeshughulikia Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angellah Kairuki alisema Takukuru kwa kushirikiana na taasisi zilizo chini yake, wako njiani kuanzisha mtaala wa somo la rushwa ili ifundishwe tangu shuleni.
“Napenda kuwahakikishia waheshimiwa wabunge kwamba Serikali ya awamu ya tano haitakubali kuona rushwa ikiota mizizi. Tunaamini wanafunzi wakijengewa uwezo tangu utotoni, watachukia rushwa na hatimaye tutakuwa na Taifa lenye watu waadilifu,” amesema.
Alisema kutokana na kazi ya kupunguza watumishi hewa, hadi kufikia Aprili mwaka huu, Serikali imekwishapokea Sh bilioni 1.2 kwenye akaunti maalumu ya Takukuru iliyoko Hazina ambazo zinatokana na makusanyo kutoka kwa waliokuwa watumishi hewa.
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkazi wa UNDP, Godfrey Mulisa alisema wataendelea kushirikiana na Bunge katika miradi mbalimbali ikiwemo shughuli zinazofanywa na APNAC.
Awali, Mwenyekti wa APNAC tawi la Tanzania, George Mkuchika alisema hadi sasa wabunge wapatao 148 wamekwishajiunga na mtandao huo. Kwamba anaamini hadi Bunge hili litakapomaliza muda wake, zaidi ya robo tatu ya wabunge watakuwa wamejiunga

Rais magufuri kukabidhiwa taarifa ya kkamati ya pili ya madini ijumatatu








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk John Pombe Magufuli atapokea taarifa ya Kamati ya Pili ya wachumi na wanasheria iliyofanya uchunguzi wa madini yaliyo katika makontena yenye mchanga yaliyo katika sehemu mbalimbali nchini Jumatatu, Tarehe 12 Juni 2017, jijini Dar es Salaam.

Kamati hiyo inatarajiwa kutoa tathmini ya hasara ambayo Tanzania imeingia kutokana na mikataba ya madini, athari za kiuchumi ambazo Tanzania imezipata kutokana na mikataba ya madini na ushauri wa kisheria wa namna bora ya kuendesha migodi ya madini ambayo badala ya kuneemesha watanzania imekuwa chanzo cha umasikini kwa wananchi.
Hongera Rais kwa uamuzi wa kuwakomboa watanzania. Tukio hilo litarushwa hewani moja kwa moja (Mubashara) na vyombo mbalimbali vya radio na televisheni pamoja na mitandao ya kijamii, ikiwemo Daily News Online, Habarileo Onli

WAZEE KUPATIWA MATIBABU KWA VITAMBULISHO MAALUM



Hivi karibuni , Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na Watoto, Mh. Ummy Mwalimu  ameagiza Halmashauri zote nchini kuwaadalia na kuwapa wazee vitambulisho  vya kupata huduma za matibabu bila malipo katika hospitali , vituo vya afya na zahanati  za umma katika maeneo yao.

Waziri Ummy amewapa muda hadi kufikia Desemba 30, mwaka huu wawe wametekeleza  agizo hilo. Kwa  kuzingatia na usumbufu ambao wazee wamekuwa wakiupata wanapokwenda kupata matibabu  katika vituo vya afya utekelezaji wa agizo hilo litakuwa ni mkombozi kwao ili nao wapatiwe matibabu yanayostahili.
“Baadhi ya wazee wamekuwa wakipata tabu ya kupata huduma bora katika hospitali za umma, natoa wito kwa wakurugenzi kupunguza kadhia wanayopata wazee hao wanapokwenda kutibiwa , hakikisheni mnawapatia vitambulisho wazee wote wasiokuwa na uwezo “ alisema Waziri Ummy.
Vitambulisho hivyo vitawapa fursa ya kutibiwa bure na hivyo  watapata motisha ya kwenda kupata matibabu katika hospitali mbalimbali bila kutoa malipo yoyote. Kabla ya agizo hilo wazee kuanzia miaka 60 walikuwa wanalazimika kupata barua kutoka kwa watendaji wa Serikali za Mtaa ili waweze kutibiwa bure
Utaratibu huu kwa kiasi kikubwa ulikuwa na usumbufu ambapo walikuwa wanatakiwa kwenda kuchukua barua kwa Watendaji wa Serikali za Mitaa kila wanapoumwa  na barua hizo zilikuwa zinawawezesha kutibiwa bure kwa wakati huo na endapo wataumwa tena wanalazimika kufuata barua tena.
Serikali ilifanya uamuzi wa kuwa na Sera ya Wazee mwaka 1999, katika maadhimisho ya mwaka wa Kimataifa wa Wazee. Maamuzi hayo yalikuwa ni kielelezo cha dhamira ya Serikali  ya kuweka masuala ya wazee katika agenda za maendeleo ya nchi yetu.
 Pamoja na kuwa Serikali inawatambua wazee kuwa ni rasilimali  na hazina kubwa katika maendeleo ya nchi yetu, wazee hao wanakabiliwa  na matatizo ya umaskini, kutotosheleza kwa huduma za afya, pensheni na kutoshirikishwa katika maamuzi yanayohusu maendeleo ya nchi yetu. Wazee wengi huishi katika hali ya umaskini  inayoleta mashaka makubwa kwao na takribani  asilimia 75 wazee wanaishi vijijini.
 Taarifa za Umoja wa Mataifa  za mwaka 1999, zinaonyesha kuwa  katika Afrika , Tanzania ni nchi ya pili kuwa na sera ya wazee baada  ya nchi ya Mauritius.
Kupitia Sera hiyo Serikali iliahidi kuhakikisha kuwa wazee wanatambuliwa na wanapata fursa  ya kushiriki katika maendeleo ya nchi sambamba na wananchi wengine.
Aidha taarifa hizo zinaendelea kuonyesha kuwa  kumekuwa na ongezeko la  idadi ya wazee duniani na hasa katika nchi zinazoendelea ambapo viwango vya ongezeko havilingani na uwezo wa rasilimali zilizopo kuwahudumia katika nyanja za afya, lishe, na huduma nyingine za msingi kwa maisha ya binadamu.
Takwimu zinaonyesha kuwa mwaka 1950, Umoja wa Mataifa ulikadiria kuwepo kwa watu milioni 200 wenye umri zaidi ya miaka 60, na mwaka 1975, idadi iliongezeka kufikia milioni 350 na ilitegemea kuongezeka kufikia milioni 625, ifikapo mwaka 2005 na idadi hiyo itazidi idadi ya vijana na watoto wenye umri wa miaka 24 ifikapo mwaka 2050.
Barani Afrika idadi inategemea kuongezeka kutoka milioni 38 za mwaka 1999, na kufikia milioni 212 ifikapo  mwaka 2050. Kwa kuangalia ongezeko hilo la wazee  ni wakati muafaka wa kuwapatia vitambulisho ili kuwapunguzia adha ya kupata huduma za afya.
Sera ya Taifa ya Afya na Sheria ya Utumishi wa Umma nchini Tanzania zinazingatia umri wa miaka 60 kuwa ndio kigezo  cha uzee , hivyo kwa sera hii mzee ni mtu mwenye wa miaka 60 na kuendelea. Madhumuni ya sera hii ni pamoja na kuwatambua kama rasilimali muhimu katika maendeleo ya Taifa letu na kuhakikisha kuwa wazee wanapata huduma zote za msingi zikiwemo huduma za afya.
Nchini Tanzania wazee wapo katika makundi mbalimbali ambayo ni wazee wastaafu, wakulima, wafugaji wavuvi na wale wasio na ajira ambao kuzeeka kwao ni matokeo ya kupungukiwa nguvu za kufanya kazi.
Mazingira ya wazee hao ni pamoja na matunzo duni,  umaskini, magonjwa  ya muda mrefu, lishe duni , huduma za afya kuwa ghali na wao kushindwa kuzimudu, na kuhitaji uangalizi na matunzo maalum  ya kitaalamu.
Kwa kuanzisha utaratibu wa kutoa vitambulisho vya matibabu kwa wazee , Serkali imetekeleza ahadi  ya kurekebisha Sera  ya kuchangia gharama za afya kwa kurekebisha vigezo vya utambuzi wa umri wa miaka 60 na kuweka utaratibu wa kufuatilia afya za wazee katika jamii.
Wazee wote wenye sifa za kuwa na vitambulisho hivyo ni budi wajitokeze kwa wingi ili waweze kupatiwa  na kuwaondolea kabisa adha ya kupata huduma za matibabu katika hospitali za umma.

SERIKALI: MARUFUKU KUTUMA VIFURUSHI KAMPUNI BINAFSI


 

 SERIKALI imepiga marufuku taasisi za umma kutuma mizigo au vifurushi kwa kutumia kampuni binafsi za usafirishaji, badala yake zitumie Shirika la Posta Tanzania (TPC), ikidai ni kuziba mianya ya upotevu wa fedha.

Agizo hilo lilitolewa   hivi karibuni na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, wakati akizungumza na watumishi walio chini ya wizara hiyo katika kikao maalumu kilichofanyika jijini Mwanza.


Katika kuhakikisha agizo hilo linatekelezwa  ipasavyo pamoja na mambo mengine ya maadili ya kiutumishi, Profesa Mbarawa aliamua kutoa namba zake za simu za mkononi; 0622000001 na 0686955116 ili kuwasiliana naye pale itakapobainika mtumishi anafanya vitendo kinyume na taratibu za kazi.

“Shirika letu lazima lifufuliwe ili lipate mafanikio, hili tutalisimamia kweli kweli na naomba watu tuzingatie maagizo, kama Serikali  tunaendelea kufanya maboresho kuanzia kwa watumishi wa kawaida hadi kwa postamkuu,  kikubwa ni kufanya kazi kwa bidii kwa kuzingatia sheria,” alisema.

Profesa Mbarawa pia aligusia juu ya mali za TTCL na kuahidi kuanza kuzifuatilia kwani alidai wapo baadhi ya waliopanga kwenye majengo la shirika hilo lakini nao wanapangisha wengine.

Alisema  hadi sasa majengo  ya TTCL hayana tija kwa shirika kutokana na udalali unaofanyika na kuwataka viongozi kuanza kupitia mikataba upya kabla ya wizara kuanza  uchunguzi.

W AZIRI AOMBA DINI ZIELIMISHE KUHUSU MITANDAO YA KIJAMII






VIONGOZI wa dini nchini wametakiwa kutumia nafasi zao kuelimisha umma kuhusu matumizi sahihi ya huduma ya mitandao ya kijamii ili kujiletea maendeleo.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa wakati wa futari iliyoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kushirikiana na Kamati ya Amani ya Mkoa wa Dar es Salaam.
Alisema ni vema viongozi wakatumia nafasi zao kueleza matumizi sahihi na huduma za mitandao ya kijamii katika kueneza imani na kujiletea maendeleo binafsi na taifa kwa jumla.
Waziri Mbarawa alitoa mfano wa machafuko ya nchi ya Misri ya mwaka 2011 yaliyodumu hadi sasa kuwa yametokana na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii kutokana na ujumbe wa mtu mmoja aliouandika kwenye ukurasa wake wa Facebook.
Mwenyekiti wa Kamati ya Amani ya Mkoa wa Dar es Salaam, Shehe Alhad Mussa Salum alisema Kamati yao imefanya mambo mengi kuhakikisha kunakuwapo amani na utulivu nchini.
Shehe Salum alitumia fursa hiyo kuwataka Waislamu kutumia kipindi cha Mfungo wa Mwezi Mtukufu Ramadhan kuleta amani miongoni mwa watu wa imani na dini mbalimbali. Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, James Kilaba alisema ukuaji wa teknolojia umekuja na changamoto nyingi zinazohitaji ushirikiano na wadau mbalimbali kuzishughulikia.
B ANNA, SAKAYA WAFURAHIA BULAYA, MDEE KUTIMULIWA BUNGE

B ANNA, SAKAYA WAFURAHIA BULAYA, MDEE KUTIMULIWA BUNGE



                                                   

MHADHIRI Mwandamizi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Benson Banna, amesema adhabu iliyotolewa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa wabunge wawili wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Halima Mdee na Ester Bulaya ya kufungiwa shughuli za Bunge kwa takriban mwaka mmoja ni sahihi.

Wabunge hao walipewa adhabu hiyo juzi kwa kosa la utovu wa nidhamu katika kikao cha Bunge na kukidharau Kiti cha Spika, Ijumaa iliyopita. Wabunge hao walionesha utovu huo wa nidhamu bungeni, wakipinga Mbunge wa Kibamba, John Mnyika kutolewa nje ya Bunge kwa agizo la Spika wa Bunge Job Ndugai.

Kutokana na Mnyika kukaidi amri ya Spika ya kumtaka akae huku Mnyika akitaka ombi lake la utaratibu bila kujali maelekezo ya Spika, Ndugai aliagiza askari kumtoa nje ya Bunge na kutohudhuria vikao vya Bunge kwa wiki moja.
Wakati askari wakimtoa Mnyika ukumbini, Halima ambaye ni mbunge wa Kawe na Bulaya wa Jimbo la Bunda Mjini, waliinuka katika viti vyao na kuelekea upande wa askari waliokuwa wakimtoa nje Mnyika huku Bulaya akihamasisha wabunge wengine wa upinzani kuondoka na kususa Bunge.

Kutokana na hali hiyo, Ndugai aliiagiza Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kujadili adhabu mwafaka na ndipo baada ya mjadala, Bunge likaridhia wabunge hao kutoshiriki shughuli za Bunge vikiwamo vikao vya Bunge na safari na vikao vya Kamati za Kudumu hadi mwezi Aprili mwakani katika Bunge la Bajeti mwaka 2018/ 2019.

Akizungumza na gazeti hili, Dk Banna alisema wabunge hao walidhalilisha Bunge, wapiga kura na wananchi katika majimbo yao. Alisema wabunge wanapaswa kuheshimu kanuni za Bunge na kuzifuata ili kufanya uwakilishi mzuri kwa wananchi.

“Kuna gharama ya kuwa Mheshimiwa na hiyo ni kuwa na hekima kwa kuwa chochote kinyume na hapo ni kosa tena kubwa na wabunge hao wamevuna kile walichokipanda,” alisema.

Mbunge wa Kaliua wa Chama cha Wananchi (CUF), Magdalena Sakaya alisema kuwa adhabu hiyo ni mwafaka kwa wabunge hao kutokana na kuwa walikwishaonywa. Alisema, Bunge linatakiwa kuheshimiwa na wabunge hao wamekuwa watata mara kwa mara katika kufuata kanuni zilizowekwa.
Alisema, wabunge wanatakiwa kuwa na nidhamu, uvumilivu na hekima ya hali ya juu kipindi chote wakati Bunge likiwa linaendelea. Alisema kwa upande wa Mdee, ndani ya kipindi kifupi amefanya makosa kadhaa ya utovu wa nidhamu.
Alisema, mbunge huyo aliitwa kwenye kikao cha Kamati ya Nidhamu mwezi Aprili baada ya kudaiwa kumtukana Spika Ndugai na alipewa karipio kali la kumtaka asirudie kosa. Alisema wakati wakiwa kwenye kikao hicho, aliambiwa wazi kuwa iwapo atarudia tena kosa, atapewa adhabu kali zaidi na kwa sasa anatumikia kile alichoonywa.

Kutetea wezi wa madini Wakati huo huo, Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde amesema kufukuzwa bungeni kwa wabunge wa Upinzani, kumetokana na kutetea wezi wa madini kwani wamekuwa wakipinga juhudi za Rais John Magufuli katika kuokoa rasilimali za Taifa yakiwamo madini.
Akizungumza kwenye Viwanja vya Bunge jana, mbunge huyo wa CCM alisema, “Mimi ndio nilikuwa nachangia na hili jambo la mchanga wa dhahabu lilikuwa linazungumziwa kipindi cha nyuma.
“Mwongozo wa Mnyika alisimama kama anatetea wezi wa mchanga wa dhahabu watu wasifikiri kuwa kuna mtu ameonewa, lakini hoja ya kutetea wezi wa dhahabu ndiyo imemgharimu Mnyika.”

Aliongeza Lusinde, “Tunajiuliza maswali ni kwabnini watu hawa walikuwa wanapinga wizi kipindi cha nyuma, lakini sasa wanatetea kuna nini kimetokea hapo katikati? “Kwa nini wanatetea wezi? Rais John Magufuli amejitahidi kuokoa madini ili fedha zitusaidie katika huduma zingine, lakini wabunge wanapinga.”

Naye Mbunge wa Mafinga Mjini, Cosato Chumi (CCM) alisema, “Tulikuwa tunajadili mchanga wa dhahabu sasa tunapongeza hatua alizochukua rais, lakini watu ambao walikuwa wanazungumzia suala hilo kwa miaka mingi wanaanza kupinga, hapa lazima tuhisi kuwa kuna kitu huenda wamepewa na hao wezi.”

Alieleza kuwa haiingii akilini kwa wabunge ambao ni wazalendo kupinga juhudi zinazofanywa na Rais kama hawajapewa fedha yoyote na hao waliokuwa wanaliibia taifa. “Ifike mahala tuseme ukweli katika hili uzalendo ulitakiwa kwani tuliibiwa taifa na hiki ndicho kimefanya Mnyika aadhibiwe kwa kuwa alitetea wezi na ndicho chanzo na mbunge mwingine kuropoka kuwa ni mwizi kwa sababu haeleweki,” alieleza Chumi.

Alisema hata adhabu waliopewa wabunge Halima Mdee (Kawe) na Ester Bulaya (Bunda Mjini), chanzo chake ni kumtetea John Mnyika aliyekuwa anatetea wizi unaofanywa na kampuni za madini, jambo ambalo halikubaliki na kuwaomba wabunge kuungana katika kushughulikia mambo ya kitaifa.
Mbunge wa Chemba, Juma Nkamia (CCM) alisema wabunge hao wa Upinzani wanapaswa kuheshimu mamlaka inayoongoza Bunge. “Waache waende. Pale bungeni kuna viongozi wetu, ni lazima kuwaheshimu. Kuheshimu mamlaka ni muhimu na ni lazima,” alieleza Naibu Waziri huyo wa zamani.
Juzi, Bunge kwa pamoja, lilipitisha adhabu ya kusimamishwa kwa mikutano mitatu wabunge wa Chadema, Mdee na Bulaya kutokana na utovu wa nidhamu na kutoheshimu mamlaka ya Spika.

Hawatahudhuria mikutano ya Bunge kuanzia juzi katika Mkutano wa Saba unaoendelea, Mkutano wa Nane mwezi Novemba na ule wa Tisa Februari mwakani. Watarejea bungeni Aprili mwakani wakati wa Mkutano wa Bunge la Bajeti, na muda wote huo hawataruhusiwa kushiriki shughuli zozote za kibunge.

Kiini cha kufungiwa kwao ni vurugu zilizotokea wakati Lusinde akichangia Bajeti ya Nishati na Madini, ambako alikatizwa na Mnyika aliyekuwa akitaka Spika achukue hatua dhidi ya mbunge aliyedai amemwita mwizi.

Katika hotuba yake ya Kambi ya Upinzani kwa bajeti hiyo, Mnyika alipinga ripoti ya Kamati ya Rais Magufuli ya uchunguzi wa makinikia, kiasi cha wabunge wengine kuhoji upinzani wana ajenda gani na kueleza kuwa wanatumiwa na waliofilisi nchini katika sekta ya madini.


Kategori

Kategori