FIGHT FOR FREEDOM

FIGHT FOR FREEDOM

ZIJUE SABABU ZA KIHARUSI KUPOOZA AU STROKE

Ni dhahiri kuwa wagonjwa wengi siku hizi wamekuwa wakikumbwa na tatizo hili la kupooza ambalo wengi huwakumba ghafla wakiwa hawana ufahamu wowote nini ambacho kimetokea.

Kabla zijakuelimisha mengi mpendwa msomaji wangu wa Makala zangu, basi leo nakupa maana ya baadhi ya maneno haya:

Kupooza
Hii ni ile hali ya kiungo kupoteza utendaji kazi wake kwa sababu ya neva za fahamu kuathiriwa.

Kiharusi au stroke
Hii ni ile hali ya ubongo kupata hitilafu katika kupokea damu na hatimaye kupelekea kupooza kwa viungo baadhi au mwili mzima. Na endapo seli za ubongo zikikosa damu na oksijeni kwa dakika 3 zinaanza kufa na kupoteza utendaji kazi wake na endapo hili tatizo lisipo shughurikiwa ndani ya masaa matatu dalili zake zinakuwa zimefikia pabaya sana katika matibabu.

Sasa basi ningependa kuongelea kidogo kuhusu ugonjwa huu na jinsi gani unaweza kujizuia.

Sababu zisizo epukika
Napenda kusema kwamba, Katika kitabu cha The China Study kilicho andikwa na Prof. Collin Campbell kinasema kwamba, kila binadamu ana chembe chembe za vina saba yani DNA za urithi kutoka kwa wazazi wetu ambazo zinarithishwa kila kizazi.

Hivyo kila mtu ana viini vya urithi vya magonjwa mbalimbali kutoka kwa wazazi wetu, ni jukumu lako kufanya chembe chembe hizo zijioneshe wazi wazi. Hivyo bwana Campbell ambaye ni mtafiti mashuhuri wa lishe na magonjwa alisema kuwa, ni jukumu lako wewe kuuchokoza mwili wako uwezo kuonesha magonjwa ambayo umeyarithi kutoka katika ukoo wenu.

Endapo ukiishi maisha ya kiafya, kula vizuri vyakula vya asili hutasumbuka na magonjwa kama kisukari,shinikizo la damu,uvimbe kwenye kizazi,ugumba,kansa nk.
Kwa sababu tumeshindwa kuishi maisha ya uhalisia wetu, tunaishi kwa kufurahia vyakula vilivyofanyiwa marekebisho na binadamu na kufurahia bei yake ilivyo ndogo katika kiwango cha kujitosheleza, Basi swali la kujiuliza ni kwa nini vyakula hivyo vya viwandani vinauzwa bei ya chini sana kuzidi vyakula asili? Hebu nenda leo ukanunue nyanya ambazo unaweza kukamua ukapata chupa moja ya 400mls! UTAGHARIMIKA PESA KUBWA KULIKO YULE ALIYENUNUA Nyanya iliyotengenezwa kiwandani na kuwekwa kwenye chupa maalumu, Jiulize tena Kwa nini vinauzwa bei ya kiwango cha chini kiasi hicho?

Mwenendo huo wa maisha ya ulaji vyakula vya viwandani, vinywaji vyenye sukari nyingi, radha, rangi, unatufanya tuwe na vihatarishi vya kupata ugonjwa wa kupoooza bila kuwa na uwezo wa kuepuka hadi pale tutakapo badili mwenendo wa maisha yetu.

UMRI
Tafiti zinaonesha kuwa kadri umri wako unavyozidi kuwa mkubwa ndivyo unavyozidi kuwa hatarini sana kukumbwa na tatizo la kupooza. Umri Zaidi ya miaka 50 upo katika hatari kubwa sana ya kupata magonjwa yatakayokupelekea kupata kiharusi. Kwani kiharusi ni ugonjwa moja wapo utakao kupelekea kupooza kwa baadhi ya viungo vya mwili wako na haimaye mwili mzima.

Hivyo kama wewe bado hujafikia katika umri huu, basi ni wakati wa kuishi katika lishe asili  Inatoka katika mashamba yetu ya wakulima.

JINSIA
Tafiti zinaonesha kwamba wanaume wako hatarini sana kupata kiharusi ukilinganisha na jinsia ya kike. Lakini pia tafiti zinaonesha kuwa kati ya mwanamke na mwanaume, mwanamke ndiye yupo hatarini sana kupata kifo kitokanacho na kiharusi. Hivyo endapo mwanamke akipatwa na kiharusi maendeleo yake kuanzia anapopatwa na tatizo huwa sio mazuri sana ukilinganisha na mwanaume. Hivyo mwanamke huwahi kukutwa na kifo Zaidi ukilinganisha na mwanaume anaweza kukaa muda mrefu sana.

URITHI
Kuna watu wenye historia kuwa katika ukoo wao kuna watu wenye matatizo ya kiharusi au babu, bibi alikumbwa na tatizo hilo. Hivyo hata wewe unaweza ukawa hatarini kupata tatizo kama hilo endapo tu maisha unayoishi nayo yakiwa ni maisha yasiyo jumuisha lishe ya asili ninayopenda kuita lishe ya dawa.

KAMA UMESHAWAHI KUPATWA KIHARUSI KIDOGO
Hii ni aina ya kiharusi inayotokea kwa muda mfupi na kupotea. Muda mwingine huwa ni vigumu kutofautisha na kiharusi chenyewe. Maana kiharusi kidogo (Transient Ischemic Attach) husababisha pia viungo kupoteza utendaji kazi wake na inaweza pia kuathiri utendaji kazi wa ubongo kiakiri pia. Hivyo kama umeshawahi patwa na TIA kipindi cha nyuma, uwezekano wa kupata tena ni mkubwa sana, na unaweza kupata kiharusi kabisa chenyewe.
Hapo juu nimesema kuwa ni vihatarishi visivyozuilika LAKINI ni kwa wale wasioweza kubadili mienendo ya maisha ya kifahari na kujiepusha na magonjwa tabia kama kisukari,shinikizo la damu na kiwango kikubwa cha lehemu mwilini mwako

Sababu unazowezo kuzisababisha wewe mwenyewe na kukupelekea kupata kiharusi ( stroke)

Magonjwa ya moyo
Magonjwa ya moyo kwa umri Zaidi ya miaka 60 imekuwa ni kawaida kutokana na miili yetu kuwa na kiwango kikubwa cha sumu mwilini mwetu na miili yetu kuwepo katika mazingira ya kupokea vyakula visivyo vya msingi katika kuboresha utendaji kazi wa mwili wako na tofauti na kuharibu uwezo wa mwili wako kufanya kazi ipasavyo.

Moja wapo ya magonjwa yanayopelekea kupata kiharusi, ni pale moyo wako unaposhindwa kutengeneza umeme wa kutosha kutoka juu kwenye vyumba vya moyo viitwavyo Atria na hatimaye kusambaa kwenye vyumba vya chini vya moyo viitwavyo Ventriko.

Hivyo basi napenda kukuambia kuwa, moyo hutengeneza umeme, na umeme huo huzunguka kwenye sakiti ya umeme wa moyo, sakiti hio huanzia kwenye vyumba vya juu vya moyo na kushuka vyumba vya chini na hatimaye kusambaa katika misuli yote ya moyo na hatimaye kusukuma damu kutoka kwenye moyo.

Hivyo kunapokuwa kuna hitirafu katika utengenezwaji wa umeme kuanzia sehemu husika, umeme unatengenezwa usiotosheleza na unatoka sehemu mbalimbali (sio maalumu) unajikuta misuli ya moyo inapata umeme kutoka katika vyanzo tofauti na umeme huo hautoshelezi kuweza kusukuma damu ipasavyo. Ugonjwa huu kwa lugha ya kiratini tunaita Atrial Fibrillation. H

ivyo moyo wako unapokuwa na tatizo hili, hata mapigo ya moyo hubadirika. Njia pekee ambayo unaweza ukajigundua kuwa una tatizo hili, ni kuangalia kiashiria cha mapigo ya moyo sehemu mbali mbali kama shingoni,juu ya mkoni wako karibu na kiganja kama mapigo ya moyo yanaenda sawa au laa! Pia unaweza kwenda Zaidi kufanya uchunguzi kama kipimo cha ELECTROCARDIOGRAM (ECG) unaweza kupata majibu halisi kuwa umeme huo unajitosheleza au laa! Na unatengenezwa kutoka katika chanzo kimoja au laa! Pia moja ya sababu moja wapo ni kuangalia misuli ya moyo na kiwango cha damu kinachosukumwa na myo wako, ni vyema pia ukipata kipimo kingine cha moyo kinaitwa ECHOCARDIOGRAM(ECHO) hiki kinakupa taarifa zote za kiwango cha damu kinachosukumwa,ukubwa wa misuli ya moyo, na taarifa zinginezo. Kumbuka vipimo hivi vinapatikana katika hospitali kubwa za rufaa na vinategemea umahili wa mpimaji na msomaji wa majibu yako.

Ugonjwa huu wa moyo unaweza kusababisha kiharusi kwa sababu moja kuu kwamba, pale moyo unaposhindwa kutenegeneza umeme wa kutosha kusukuma damu, kutakuwa na mrundikano wa tamu kwenye moyo na damu hio inaweza kuganda na hatimaye kusukumwa kwenda kwenye mishipa midogo ya ubongo na kusababisha kizuizi cha damu kufika kwenye ubongo kwa sababu ya kutwama kwa damu iliyo ganda. Hivyo ndivyo unaweza kupata kiharusi endapo moyo wako hautengenezi vizuri umeme wake.

Kiwango kingi cha cholestero(lehemu) mbaya mwilini mwako
Lehemu kwa tafsiri nyepesi ni fati(mafuta) ambayo ipo kama nta ( wax) huzunguka sehmu mbalimbali katika mwili wako kwa kupitia mfumo wa mzunguko wa damu.
Ikumbukwe Lehemu ina kazi kubwa sana miilini mwetu kama kutengeneza seli za mwili na kutengeneza homoni za miili yetu na kazi zingine nyingi. Hivyo basi ningependa kukuambia kuwa kuna ina kuu tatu za lehemu ambazo ningependa kuzitaja kwa ufupi katika makundi makuu mawili, Lehemu mbaya ambayo inajulikana kama Low density Lipoprotein (LDL)  pia na Triglycerides na aina ya pili ni lehemu nzuri ijuilikanayo kama Hingh density Lipoprotein –HDL.

Lehemu inaweza kusababisha kiharusi kwa sababu ya tabia yake mbaya ya kunasa kiurahisi kwenye kuta za mishipa ya ateri na hatimaye kupunguza kipenyo cha mshipa wa damu au kuziba kabisa na hatimaye kuzuia damu kufika vizuri katika ubongo na hatimaye ubongo hukosa damu na oxygen.

Tafiti zinaonesha kwamba ulaji wa nyama za aina yoyote ile, zina kiwango kingi sana cha lehemu mbaya ambayo inaenda kutuathiri sana. Lakini pia tafiti zinaonesha kwamba ulaji wa vyakula vya mboga za majani, matunda vinasaidia sana kuepukana na lehemu mbaya na kumaliza kabisa matatizo yanayo sababishwa na lehemu mbaya mwilini mwako.

Rehemu hujulikana kama kisababishi kikubwa cha aina moja wapo ya kiharusi kinachosababishwa na mishipa midogo ya damu kutopitisha damu na kuulisha ubongo wako vizuri na hatimaye seli za ubongo huanza kufa nah ii hutokea baada tu ya ubongo kukosa damu kwa muda wa dakika tatu.

Aina hii ya kiharusi huitwa ISCHEMIC STROKE (Ischemia, Ni ile hali cha seli za mwili kufa Kwa kukosa oxygen, na Stroke ni kupooza). Hivyo Ischemic stroke ni kupooza kunako sababishwa na kukosa hewa ya oksijeni kwenye ubongo kwa sababu ya kukosa damu kwenye ubongo kunakosababishwa na kuziba kwa mishipa midogo midogo inayopeleka damu kwenye ubongo.
Unaweza kuchunguza kiwango chako cha lehemu kama kingi au laa! Unaweza kwa kuchunguza kitalamu kwa kuchukua sampuli ya damu na kupeleka maabala (Biochemistry Lab) na hatimaye utapata majibu yako. Pia unaweza ukatumia vipimo vingine vya picha vinavyopima kiwango cha lehemu mbaya moja kwa moja kwenye mishipa ya damu Angiogram na pia unaweza kupima kwa kutumia Kipimo cha kuangalia uzalishaji wa umeme kwenye moyo kwani lehemu ni chanzo kikubwa sana cha kuharibu utendaji kazi wa moyo hivyo kipimo cha Electrocardiogram kinaweza pia kutumika na kuangalia moja kwa moja.

Note: Napenda kutoa angalizo kuwa vipimo vingi ninavyotaja hapo ni vikubwa sana na gharama yake kidogo kubwa na vingi vinapatikana hospitali ya rufaa na kwenye vituo mbali mbali binafsi. Na hivyo wengi wenu mmekuwa mkiniuliza kama Dr Boaz Mkumbo naweza kuwasaidia kwa hilo. Napenda kuwasaidia kama ninavyokupatia elimu hii ya afya bure kabisa, ushauri wangu ni kwamba vipimo vyote vya kitaalamu vinategemea na mpimaji na msomaji ana taaluma gani katika kusoma majibu.

Kama mpimaji akipotosha na daktari anayetibu atapotoka na hapa ndipo madhaifu makubwa ya vipimo hivi vingi na ndio maana magonjwa mengi tunashindwa kuyabaini mapema kwa kukosekana kwa ufanisi kwa watu wanaopima. Sasa ningependa kukupa siri moja ya vipimo vyote nilivyo vitaja hapo juu, Vina hitaji umahili mkubwa wa kusoma majibu, na vituo vingi binafsi havina watu mahili wa kusoma vipimo hivi ,viko pale kama kitega uchumi kukushusha roho kuwa umepima.

Tatizo sio kupima, Kiu ni kugundua ugonjwa sahihi na utibiwe upone. Ningependa kukushauiri kama unahitaji vipimo hivi, fika hospitali yenye wataalamu wa kutosha wenye uwezo mkubwa wa kukupa majibu ya uhakika ya kukata kiu yako.
American Diabetes Association Inashauri kiwango cha LDL cholesterol kuwa chini ya 100 mg/dl kwa watu wenye kisukari na chini ya 70 mg/dl kwa watu wenye magonjwa ya moyo.
Pia inashauri kuwa kiwango cha lehemu nzuri yani HDL iwe 50 mg/dl au Zaidi kwa wanawake na kwa wanaume HDL iwe 40 mg/dl au Zaidi.

Shinikizo la juu la damu( high blood pressure)
Shinikizo la damu ni msukumo wa damu ndani ya mishipa ya damu thidi ya ukuta wa mishipa. Shinikizo la damu lenye takwimu ya Zaidi 140/90 mmhg kwa muda mrefu utakuwa unastahili kuitwa mgonjwa wa shinikizo la juu la damu.

Shinikizo kubwa la damu husababisha kiharusi kwa kusababisha mishipa midogo ya damu ya ubongo kupasuka na hatimaye damu kuvia kwenye ubongo. Aina hii ya kiharusi huitwa Hemorrhegic Stroke. Aina hii ya kiharusi ni mara chache sana kutokea na huwa ni nadra sana kukuta mtu ana aina hii ya kiharusi lakini ndio aina nambari moja inayoweza kusababisha kifo haraka sana kwa mgonjwa. Kwani wagonjwa wengi wanaopata aina hii ya kiharusi huwa maendeleo yao sio mazuri na wengi hufika hospitali wakiwa hawajitambui kabisa.

Ugonjwa wa Shinikizo la damu unazuilika kabisa kwa kufuata masharti machache kama haya hapa chini:
Ulaji wa vyakula vya madini ya potasiamu hadi kufikia 3900mg kwa siku kutoka kwenye ndizi,machungwa,matunda yaliyo kaushwa,viazi vitamu nk
Ulaji wa Madini ya Calcium angalau 1200mg kila siku kutoka kwenye vyakula kama mtindi na maziwa ya kuwaida,Ulaji wa vyakula vyenye magnesium angalau 420mg kwa siku kwa wanaume na 320mg kwa wanawake kutoka kwenye vyakula kama Spinachi, nafaka isiyokobolewa, Ndizi nk

Kutofanya mazoezi ya viungo
Mazoezi siku hizi yamekuwa yakitumiwa na watu pekee wanao hitaji kupunguza mwili na kupunguza nyama uzembe ( belly fats) ,inapendeza sana wadada wengi kuchukia kubadirika kwa miili yao unaotokana na ulaji wa vyakula visivyo asili, Napenda kukuambia kuwa Mazoezi pekee sio SULUHISHO LA KUPUNGUZA MWILI WAKO, NA WALA SIO SULUHISHO LA KUONDOA NYAMA UZEMBE.

Bali siku ukijifunza kubadili mwonekano wa sahani yako mezani utafurahia jinsi uzito unavyopungua! Najua huamini, lakini unapokuwa unaanza safari ya kupunguza uzito na nyama uzembe ujue ni safari nzito kama vile safari ya kutafuta pesa. Kupungua uzito sio kurahisi ingekuwa rahisi wengi hawapendi wangekuwa wameshapungua ! Njia pekee ni kujidhatiti na kudhibutu pekee katika kubadili lishe yako, mchawi mkubwa ni sahani yako unayoiweka mbele yako kila utakapo kuweka kitu kinywani mwako.

Mazoezi huimarisha viungo na mzunguko wa damu na kusaidia mwili wako kutoa taka ambazo zimepatikana kutokana na shughuli za mwili.
Tafiti zinaonesha kwamba watu ambao hawafanyi mazoezi ya kutosha katika umri mkubwa huwa hatarini kupata kiharusi aina ya Ishemic stroke inayosababishwa na damu kutosukumwa ipasavyo katika mishipa ya damu na kusababisha  emboli kunasa kwenye mishipa ya damu na kuzuia damu kufika vizuri katika ubongo.